Sunday, October 15, 2006

SHAIRI LA KUOWA

[1]

Owa s'andame hadaa, moyo ukahadaiwa
Owa anaye kufaa, mke mwenye kusifiwa
Owa upate kuzaa, kama ulivyozaliwa
Owa ukijaaliwa, mupendane na mkeo

[2]

Owa aliye na kheri, muandamane kwa dini
Owa yai la johari, litiye nuru nyumbani
Owa mdomo mzuri, ukupambie lisani
Owa ungiye nyumbani, mupendane na mkeo

[3]

Owa moyo wa imani, usozumbua mafuja
Owa usiowe duni, anayeitwa kioja
Owa mtenda wa dini, ndiye mke mwenye haja
Owa utungiwe koja, mupendane na mkeo

[4]

Owa siowe tambara, linukiyalo vibaya
Owa mwanamke jura, mlekeze njema ndia
Owa usiowe sura, kutaka kuzangaliya
Owa mzuri tabiya, mupendane na mkeo

[5]

Owa kijana kitoto, mteshi wa kutekeya
Owa akwandike jito, mwenye kukuhurumiya
Owa usiowe zito, jabali likakwemeya
Owa aliye na haya, mupendane na mkeo

[6]

Owa s'andame uhuni, upate juwa kuzawa
Owa nami natamani, ela sijajaaliwa
Owa utiye chandani, pete uloiteuwa
Owa ujuwe kuowa, mupendane na mkeo

[7]

Owa uvishwe kilemba, na joho na mahazamu
Owa wapate kupamba, ukale twiba na tamu
Owa upambiwe chumba, upate tanganya damu
Owa usijidhulumu, mupendane na mkeo

[8]

Owa kinda la tausi, alo nadhifu mibele
Owa kiini cheusi, chendacho nyuma na mbele
Owa siowe tetesi, apaye watu uwele
Owa aliye lekele, mupendane na mkeo

[9]

Owa ualike watu, wahudhuriye arusi
Owa nawe uwe mtu, mkeo simnakisi
Owa muonyane utu, mukae mutaanasi
Owa mupane mepesi, mupendane na mkeo

[10]

Owa akukubaliye, akuizao siowe
Owa upendane naye, zamani sizo ujuwe
Owa akuridhiyae, mujikubali wenyewe
Owa mukae mutuwe, mupendane na mkeo

[11]

Owa chenye asimini, kikuba cha asiliya
Owa kilo na rihani, na waridi maridhiya
Owa kilicho na shani, na manukato kutiya
Owa ujuwe duniya, mupendane na mkeo

[12]

Owa utukuze cheo, na jina lipate kuwa
Owa apate mkeo, aambiwe meolewa
Owa kama waowao, moyo usiliye ngowa
Owa ujuwe kukuwa, mupendane na mkeo

(BY AHMAD NASSIR FROM THE BOOK "MALENGA WA MVITA")

1 comment:

bhaddy shee, Amu. said...

Ahmad Nassir Malenga wa Mvita!